Waziri wa Mambo ya Ndani nchini Tanzania, Kangi Lugola, amewataka polisi kukoma kuwanyima watuhumiwa dhamana hasa siku za mapumziko, kwa kisingizio kuwa si siku za kazi.
Waziri huyo alisema jambo hilo ni kinyume cha sheria na mtu yeyote anayestahiki kupewa dhamana anafaa kuhudumiwa katika chini ya saa 24 wakati wowote ule.
Bw Lugola alisema hayo katika kijiji cha Busanza wilayani Uvinza mkoani Kigoma siku ya Jumapili.
Aidha, aliwataka wananchi watakaoombwa fedha ili wapewe dhamana kuripoti tukio hilo kwa maofisa wa ngazi za juu ili askari husika achukuliwe hatua za kinidhamu.
"Kuna tabia iliyozoeleka katika jamii, eti kuingia polisi ni bure ila kutoka ni fedha, hii kauli nataka ife kwa sababu nawajua polisi na hawanidanganyi kwa lolote," amesema.